Jumamosi, 5 Oktoba 2013

USIKOSE KUONA KINACHOENDELEA MOJA KWA MOJA PALE ARUSHA MECHI KATI YA MBEYA CITY NA JKT ALJORO


 MEZA KUU WAKIWA WANANGOJA KUTAZAMA MPIRA 
 TIMU ZOTE MBILI ZIKIWA ZINAINGIA UWANJANI
 MGENI RASMI  AKIWA ANAKAGUA TIMU ZOTE MBILI
 MA NAHODHA WA TIMU ZOTE MBILI WAKIWA WANACHAGUA WAANZIE KUKAA GOLI LIPI
 KIKOSI CHA JKT OLJORO FC WAKIWA KATIKA PICHA YA PAMOJA
 KIKOSI CHA MBEYA CITY FC WAKIWA WANAOMBA DUA
 KIKOSI CHA MBEYA CITY FC WAKIWA KATIKA PICHA YA PAMOJA
 KOCHA WA TIMU YA MBEYA CITY FC  WA KWANZA AKIWA ANATAZAMA MPIRA KWA MAKINI
 TIMU YA MBEYA CITY FC WAKIWA WANAWASHUKURU MASHABIKI 
 MASHABIKI WA MBEYA CITY FC
 MASHABIKI MBALIMBALI 
 MASHABIKI WA JKT OLJORO NAO HAWAPO NYUMA
 MPIRA UKIWA UMEANZA
TIMU YA MBEYA CITY FC WAKIWA WANASHANGILIA GOLI LA KWANZA LILILO FUNGWA NA PAULO NONGA (26) DAKIKA YA 20
MASHABIKI WA MBEYA CITY FC WAKIWA WANASHANGILIA GOLI LA KWANZA

ENDELEA KUFUATILIA . 

MOTO WA MBEYA CITY WAWATIA PRESHA TIMU YA JKT OLJORO FC...HAPA MASHABIKI WANAONEKANA WAKIWA WAMEFUNGA BARABARA JIJINI ARUSHA

HIVI NDIVYO HALI HALISI ILIVYO SASA JIJINI ARUSHA AMBAPO MASHABIKI WA MBEYA CITY FC WAMEFUNGA BARABARA WAKIWA WANAELEKEA UWANJANI KWA AJILI YA KUSHABIKIA TIMU YAO....

HOTUBA YA RAIS KIKWETE KWA WANANCHI 04 OCT 2013.

 

Ndugu Wananchi;

          Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujaalia uzima na kutuwezesha kumaliza mwezi Septemba salama na kuwasiliana kwa kutumia utaratibu wetu huu mzuri.Naomba radhi kuzungumza nanyi siku ya leo kwa sababu nilikuwa safari na nilirejea jioni ya tarehe 30 Septemba, 2013.


Awali nilifikiria nisiseme, nisubiri mwisho wa mwezi wa Oktoba.  Lakini, baada ya kupata taarifa ya yaliyojiri, nimeshauriwa na nimekubali angalau niyasemee baadhi ya mambo huenda itasaidia.  Niwieni radhi nisipoyasemea baadhi ya mambo siyo kwa kuyapuuza, bali kwa kuepuka hotuba kuwa ndefu mno.  Nitayatafutia mahali pengine pa kuyasemea.

Uhusiano na Rwanda

Ndugu Wananchi;

          Katika hotuba yangu ya mwisho wa mwezi wa Julai, nilizungumzia hali ya uhusiano wetu na Rwanda kutokuwa mzuri na tatizo la ujambazi na wahamiaji haramu katika Mikoa ya Kigoma, Geita na Kagera.  Nafurahi kusema kuwa kwa yote mawili kuna maendeleo ya kutia moyo.

          Tarehe 5 Septemba, 2013, nilikutana na kuzungumza na Mheshimiwa Rais Paul Kagame wa Rwanda mjini Kampala.  Tuliitumia fursa ya ushiriki wetu katika Mkutano wa Nchi za Maziwa Makuu kuzungumzia uhusiano baina yetu na nchi zetu.  Mazungumzo yalikuwa mazuri na sote tulikubaliana kuwa yaliyopita si ndwele tugange yajayo.  Kwa sababu hiyo tulielewana kuwa tutengeneze mazingira yatakayosaidia kutuliza hali na kurudisha nchi zetu katika uhusiano mwema kama ilivyokuwa siku zote.  Nawaomba ndugu zangu hususan wanasiasa, watumishi wa umma, wanahabari na wenye mitandao ya kijamii na blog na wananchi kwa ujumla tusaidie kuimarisha uhusiano mwema baina ya Rwanda na Tanzania na watu wake.

Majambazi na Wahamiaji Haramu

Ndugu Wananchi;

Katika hotuba hiyo pia nilisema kuwa tutachukua hatua thabiti dhidi ya majambazi na wageni wanaoishi nchini bila ya kuzingatia taratibu zinazohusika.  Niliwataka majambazi wajisalimishe wao na silaha zao kwa hiari.  Wale wanaoishi nchini bila ya kuwa na kibali halali wahalalishe ukaazi wao au warejee makwao.  Nilitoa siku 14 kuanzia tarehe 29 Agosti, 2013 wafanye hivyo kwani baada ya hapo tungeanzisha operesheni maalum ya kushughulika na watu wa makundi yote mawili.

Ndugu Wananchi;

          Kumekuwepo na mafanikio ya kutia moyo.  Kwa upande wa wahamiaji wanaoishi nchini kinyume cha sheria watu wapatao 21,254 waliondoka kwa hiari.  Hali kadhalika zaidi ya ng’ombe 8,000 waliondolewa na silaha 102 zilisalimishwa.   Baada ya operesheni kuanza tarehe 6 Septemba, 2013 na kumalizika tarehe 20 Septemba, 2013, wahamiaji haramu 12,828 walirejeshwa makwao na watuhumiwa 279 wa unyang’anyi wa kutumia silaha walikamatwa.  Aidha, mabomu 10 ya kutupa kwa mkono (offensive hand grenades), silaha 80, risasi 780 na mitambo 2 ya kutengeneza magobole vilikamatwa.  Pia, ng’ombe 8,226 walikamatwa wakichungwa katika mapori ya hifadhi.  Kwa upande wa mazao ya misitu, mbao 2,105 zilikamatwa pamoja na nyara mbalimbali za Serikali.

Ndugu Wananchi;

          Agizo la kuwataka watu wanaoishi nchini isivyo halali wahalalishe ukaazi wao au waondoke kwa hiari au wataondolewa lilipotoshwa hasa na vyombo vya habari vya nje ya Tanzania.  Walikuwa wanadai eti Tanzania ilikuwa inafukuza wakimbizi.  Madai hayo si ya kweli hata kidogo.   Hadi kufikia tarehe 30 Septemba, 2013 wakimbizi 68,711 walikuwepo kwenye Kambi ya Nyarugusu, Mkoani Kigoma.  Hakuna mkimbizi ye yote aliyetakiwa kuondoka.  Ukweli ni kwamba hakuna mtu ye yote kati ya wale watu walioondoka kwa hiari au kusaidiwa kuondoka wakati wa operesheni ambaye ni mkimbizi.  Kama ingekuwa hivyo, wa kwanza kulalamika wangekuwa wenzetu wa Shirika la Wakimbizi la Umoja wa Mataifa.  Bahati nzuri jambo hilo halikutokea.

Ndugu Wananchi;

          Yalikuwepo pia madai kwamba tunawaonea na kuwatesa watu walioishi nchini miaka mingi.  Ati iweje sasa ndiyo waambiwe kuwa siyo raia.  Siku zote Serikali ilikuwa wapi? Uraia haupatikani kwa kuishi nchi ya kigeni kwa miaka mingi.  Unapatikana kwa kutimiza masharti ya kuomba na kupewa uraia.  Kama mtu hakufanya hivyo anabaki kuwa raia wa nchi aliyotoka au walikotoka wazazi wake.  Ipo mifano ya watu mashuhuri ambao walilazimika kuachia nyadhifa zao baada ya kugundulika kuwa siyo raia.  Hawakuwa wanaonewa, ndiyo matakwa ya Katiba na Sheria za nchi yetu.

Ndugu Wananchi;

          Katika kutekeleza operesheni hii niliagiza kuwa wale watu ambao wameishi hapa nchini miaka mingi ambao wana nyumba, mashamba au mali mbalimbali au wameoa au kuolewa na wana watoto au hata wajukuu waelekezwe kuhalalisha ukaazi wao.  Iwapo watakataa kufanya hivyo basi wasaidiwe kurejea kwao.  Pia niliagiza watu wasiporwe mali zao wala kudhulumiwa.  Sijapata taarifa ya kufanyika kinyume na maelekezo yangu.  Lakini kama wapo watu waliotendewa tofauti, taarifa itolewe kwa Wakuu wa Wilaya na Mikoa au hata Ofisi ya Rais ili hatua zipasazo zichukuliwe.  Hatutaki watu wadhulumiwe au kuonewa.

          Napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Waziri wa Ulinzi na JKT, Mheshimiwa Shamsi Vuai Nahodha na Waziri wa Mambo ya Ndani, Mheshimiwa Emmanuel Nchimbi kwa uongozi wao mzuri katika zoezi hili.  Pia, nawapongeza Makamanda na askari wa JWTZ na Polisi pamoja na maafisa wa Idara ya Uhamiaji, Idara ya Mifugo, Idara ya Wanyamapori, Idara ya Misitu na Idara nyinginezo za Serikali kwa kazi kubwa na nzuri waliyofanya.  Najua awamu ya kwanza imeisha tarehe 20 Septemba, 2013 na kama nilivyosema kuwa safari hii operesheni itakuwa endelevu, muda si mrefu awamu ya pili itafuata.  Nawaomba waendelee kuchapa kazi kwa bidii, maarifa na nidhamu ya hali ya juu.

Ziara ya Canada na Marekani

Ndugu Wananchi;

Kati ya tarehe 17 na 28 Septemba, 2013 nilifanya ziara ya kikazi katika nchi za Canada na Marekani.  Nchini Canada nilitembelea Chuo Kikuu cha Guelph ambapo nilitunukiwa Shahada ya Heshima ya Uzamivu kwa kutambua jitihada zetu tuzifanyazo kujiletea maendeleo na mafanikio ya kutia moyo tunayoendelea kupata licha ya changamoto zinazotukabili.  Katika mazungumzo yangu na uongozi wa chuo hicho wamekubali kuwa na ushirikiano wa karibu na Wizara zinazohusika na Elimu, Kilimo na Mifugo pamoja na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine,  Morogoro na Chuo Kikuu cha Dodoma.  Nimewataka Mawaziri wa Wizara hizo na viongozi wa vyuo hivyo kuchangamkia fursa hiyo bila kuchelewa. 

Ndugu Wananchi;

Nchini Marekani nilikutana na kuzungumza na maafisa na viongozi mbalimbali wa Serikali ya nchi hiyo wakiwemo Rais Barack Obama na baadhi ya Wabunge wa Bunge la Marekani.  Mazungumzo yetu yalilenga kuimarisha ushirikiano baina ya nchi zetu na mambo yalienda vizuri.  Wote walituhakikishia kuwa mambo tuliyoyazungumza na kukubaliana na Rais Barack Obama wakati wa ziara yake nchini yanaendelea kufanyiwa kazi.  Miongoni mwa hayo maombi yetu ya kupatiwa vitabu milioni 2.4 vya sayansi na hisabati yamekubaliwa na utekelezaji umeanza.  Upatikanaji wa vitabu hivyo utamwezesha kila mwanafunzi wa sekondari kuwa na kitabu chake.

Ndugu Wananchi;

Jambo lingine kubwa na la faraja kwetu ni kuwa mapendekezo yetu ya miradi ya umeme na barabara za vijijini za kugharamiwa na Serikali ya Marekani kupitia Shirika lao la Changamoto za Milenia yamepokelewa vizuri.  Kinachosubiriwa ni miradi ipi itakubaliwa na Bodi ya MCC na kiasi gani cha fedha kitatengwa na Bunge la Marekani kwa ajili hiyo.

Tuzo ya Uhifadhi

Jambo lingine muhimu katika safari yangu ya Marekani ni kutunukiwa tuzo na “International Congressional Conservation Foundation” kwa kutambua juhudi zetu katika kuhifadhi wanyama pori na mafanikio tuliyoyapata.  Licha ya changamoto mbalimbali tunazokabiliana nazo, tuzo hii imetupa moyo wa kuongeza nguvu katika jitihada tunazozifanya sasa kupambana na ujangili na matatizo mengine ya uhifadhi wa wanyama na misitu. 

Ndugu Wananchi;

Kilichotupa moyo zaidi ni kauli za utayari wa kutusaidia katika mapambano hayo zilizotolewa wakati wa kupewa tuzo na katika mkutano wa mfuko wa Maendeleo wa Clinton na katika mkutano maalum wa kupambana na ujangili na biashara ya meno ya tembo duniani.

Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

Ndugu Wananchi;

Shabaha kuu ya safari yangu ya Marekani ilikuwa kuhudhuria Mkutano wa 68 wa Umoja wa Mataifa unaoendelea jijini New York mpaka Desemba, 2013.  Mada kuu ya mkutano wa mwaka huu ni kuandaa agenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015 yaani: Post 2015 Development Agenda:  Setting the Stage. Kama mtakavyokumbuka Malengo ya Milenia yaliyoamuliwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2000, yanafikia ukomo wa utekelezaji wake mwaka 2015. 

Katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka huu mjadala umehusu nini kifanyike baada ya mwaka 2015.  Hata hivyo, mjadala huo unaanza kwa kufanya tathmini ya utekelezaji wa yale Malengo Manane ya Milenia ya mwaka 2000 umefikia wapi mpaka sasa na utafikia wapi mwaka 2015 kwa kila nchi na kwa dunia kwa ujumla.  Tathmini ya jumla inaonesha kuwa kumekuwepo na jitihada kubwa ya kutekeleza malengo haya katika kila nchi.  Yapo malengo ambayo utekelezaji wake umefikia shabaha hivi sasa na yapo ambayo upo uwezekano wa shabaha kufikiwa ifikapo mwaka 2015.  Vile vile yapo ambayo shabaha haitafikiwa. 

Ndugu Wananchi;

Kwa upande wetu, Tanzania, tumefikia shabaha katika mambo yafuatayo: 

 Lengo la Milenia namba 2 kuhusu uandikishaji wa watoto wenye umri wa kwenda shule ya msingi;
Lengo la Milenia namba 3 hasa kuhusu usawa wa kijinsia katika Shule za Msingi na Sekondari.  Ukweli ni kwamba, wasichana wanaanza kuwa wengi kuliko wavulana.  Hatujafikia shabaha kwa upande wa usawa wa kijinsia katika elimu ya juu na ni vigumu kulifikia ifikapo 2015.  Pia hatujafikia lengo kwa upande wa usawa wa Wabunge wanawake na wanaume.  Hata hivyo, kwa kutumia mchakato wa Katiba unaoendelea sasa tunaweza kufikia lengo katika uchaguzi wa 2015 iwapo tutaamua iwe hivyo;
Lengo la Milenia namba 4 kuhusu kupunguza idadi ya vifo vya watoto wachanga na wale wenye umri chini ya miaka mitano;
Tumefikia shabaha kwa Lengo la Milenia Namba 6 kuhusu  kupunguza maambukizi ya UKIMWI; na
Kwa upande wa lengo namba 7 kuhusu mazingira, tumefikia shabaha kwa upande wa upatikanaji wa maji mijini.  Bado tuko nyuma kwa maji vijijini ingawaje tunaweza kufikia lengo ifikapo mwaka 2015 kama tutaendeleza uwekezaji tulioamua kufanya katika bajeti ya mwaka huu.  Lakini, hatutaweza kufikia shabaha kwa upande wa usafi wa mazingira mijini na vijijini ifikapo mwaka 2015.  Safari bado ndefu sana.


Ndugu Wananchi;

Malengo ya Milenia namba 1 na namba 5 ambayo bado tuko nyuma sana ya shabaha hatutafikia lengo ifikapo 2015.  Tumeendelea kutekeleza lengo la Milenia namba 1 kuhusu kupunguza umaskini na njaa kwa zaidi ya nusu kutoka kiwango cha mwaka 2000.  Hatua tunazochukua kuleta mageuzi katika kilimo zina lengo la kuhakikisha usalama wa chakula na kuongeza mapato ya wakulima.  Mafanikio yanaanza kuonekana lakini si ya kiwango cha kutufikisha kwenye lengo ifikapo mwaka 2015.  Tunao, pia, mpango wa kupanua programu ya TASAF ya Conditional Cash Transfer ili tuwafikie watu wengi maskini.   Hata kama tutafanikiwa kuutekeleza mapema mpango huu utatusogeza sana mbele lakini bado tutakuwa chini ya lengo kwa upande wa kupunguza umaskini ifikapo 2015.

Ndugu Wananchi;

Kwa upande wa Lengo  la Milenia namba 5, kuhusu afya ya kina mama wajawazito bado tuko nyuma katika kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na kuongeza idadi ya wajawazito wanaojifungua chini ya uangalizi wa wataalamu wa afya.  Hatutaweza kufikia shabaha ifikapo mwaka 2015.  Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (2007 – 2017) una nia ya kukabiliana na matatizo haya.  Tumeongeza ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na hospitali, tumeboresha upatikanaji wa dawa na tumepanua sana mafunzo ya madaktari, wauguzi na wakunga mambo ambayo yamesaidia kutufikisha hatua tuliyopiga mpaka sasa. Naamini juhudi zetu tukiziendeleza zitatusogeza mbele zaidi ingawaje bado tutakuwa chini ya lengo.  Miaka michache ijayo, tatizo hili nalo litakuwa historia.

Ndugu Wananchi;

Lengo la Milenia namba 8 linazihusu nchi tajiri kuongeza michango yao kusaidia nchi zinazoendelea kutekeleza Malengo ya Milenia.  Bahati mbaya sana mataifa tajiri hayajafikia viwango wanavyotarajiwa kutoa na hata vile wanavyoahidi wenyewe kutoa katika majukwaa mbalimbali.  Kama wangetimiza ahadi zao, sura ya utekelezaji wa Malengo ya Milenia ingekuwa tofauti kabisa. 

Ndugu Wananchi;

Ijumaa, 4 Oktoba 2013

WAKAZI WA MBEYA WAMETOA YAO YA MOYONI...KUHUSIANA NA VURUGU ZA MBEYA

VURUGU ZA MBEYA: Kama viongozi hawajaona umuhimu wa kuwa na mashine za kutunza kumbukumbu za ahadi zao, sioni kwanini waganga njaa walazimishwe kuwa na mashine za kumbukumbu ya biashara zao





Kwa muda wa siku mbili mfululizo, jumatano na alhamisi wiki hii, jiji la Mbeya lilitawaliwa na dhahma ya moshi na milio ya mabomu ya kutoa machozi sanjari na maji ya kuwasha, kufuatia kukosekana kwa maelewano baina ya mamlaka za kiserikali kwa upande mmoja, na wafanyibiashara kwa upande wa pili. Chanzo kikuu cha sintofahamu hii kilikuwa ni mashine za kuwekea kumbukumbu sahihi za mahesabu ya kibiashara na utoaji risiti kwa bidhaa zinazouzwa (EFDs).

Filamu hii isiyo ya kufurahisha, kilikuwa tangazo la Mamlaka ya Mapato nchini (TRA), kutangaza kuwa itakapofika novemba 15, kila mfanyibiashara atatakiwa kuhakikisha kuwa amefunga mashine hiyo katika duka au sehemu yake ya biashara. Agizo ambalo liliwalenga wale wote ambao mauzo yao ni zaidi ya shilingi za kitanzania alfu arobaini na tano (45,000/=). Nirejee tena kwa herufi kubwa kuwa agizo hili liliwalenga wafanyibiashara wote ambao MAUZO yao na sio FAIDA yao kwa siku, ni kiasi hicho.

Kutokana na hali hiyo, wafanyibiashara wengi wakaanza kuhoji juu ya hilo chini chini, na siku ya Jumanne, Mkuu wa Mkoa Bw. Abbass Kandoro, baada ya kusikia manung'uniko ya wananchi wake chini chini, akaamua kuwaita viongozi wa wafanyibiashara kuwasikiliza malalamiko hayo. Kikao baina ya pande hizi mbili, kilifanyika katika ukumbi wa Mtenda, maeneo ya Soweto.

Wafanyibiashara hao wakamueleza Mkuu wa Mkoa juu ya mambo kadhaa, kubwa zaidi likiwa ni gharama za mashine hizo, ambazo zinaelezwa kuwa zinauzwa kwa gharama ya kati ya shilingi laki saba hadi nane, ambapo walihoji, iweje mfanyibiashara mwenye mtaji wa milioni mbili kwa mfano alazimishwe kununua mashine ya laki nane?
Wakahoji faida za mashine hizo ikiwa zitawasaidia kuongeza biashara zao au laa, wakitolea mfano kuwa mtu anapolipia chumba, anajua kuwa atakuwa akitunza bidhaa zake kwa kuziuza na kutengeneza faida, sasa je, mashine hizo zitawasaidia kimapato kwa namna gani? Zitawasaidia kuongeza faida kwa namna gani? Wapo ambao waliitaka serikali kama inataka kweli wao wazitumie mashine hizo, basi iwanunulie na wao hawatisita kuzitumia.

Taarifa ambazo nimezipata toka katika kinywa cha Mkuu wa Mkoa mwenyewe ni kuwa, aliyachukua malalamiko yao, kuwaahidi kuwa atayawasilisha mahali husika, na angewaita tena ili kuwajulisha nini kimetoka huko juu, na aliwaomba wafanye biashara zao kama kawaida.

Taarifa za upande wa wafanyibiashara zinaeleza kuwa, baada ya mkutano huo na RC, viongozi wa chama cha wafanyibiashara, waliona ni vyema basi wakawajulisha wenzao juu ya kilichoongelewa huko ambapo walienda wakakodi gari la matangazo, wakalipia katika mamlaka husika na kuzunguka wakitangaza mjini kuhusu uwepo wa mkutano wa wafanyibiashara katika viwanja vya Ruanda Nzovwe, maarufu pia kama CCM Ilomba, lengo likiwa kujadili suala la EFDs na kupeana mrejeshonyuma wa kikao na Mkuu wa Mkoa.

Hadi hapo kila kitu kilikaa shwari hadi pale ilipotimu siku ya jumatano asubuhi, ambapo baadhi ya wafanyibiashara walianza kukusanyika katika eneo ambako mkutano ungefanyika. Lakini wakati wakiendelea kukusanyika, ghafla gari za doria zikaanza kuonekana maeneo ya Mwanjelwa na Kabwe hadi huko Ruanda Nzovwe na kilichofuatia hapo, ndio kile ambacho kimesharipotiwa mara nyingi. Ilikuwa ni mwendo wa mabomu na machozi, maji ya kuwasha, fukuzana za kila kona, virungu kwa waliokamatwa na kila aina ya mvurugano unayoweza kuieleza.

Zaidi kuhusu tukio hili, unaweza kusoma kwa kubonyeza http://www.jukwaahuru.com/vurugu-jijini-mbeya-mkuu-wa-mkoa-aongea-na-jukwaa-huru-na-kuzielezea-a-z/ , na baada ya kujikumbusha yote haya, hebu tutafakari kwa pamoja kuwa je, tatizo hasa lilikuwa ni mashine, Polisi, TRA, wafanyibiashara au nani hasa?

Tukumbuke tu kuwa, tukio la Mbeya mjini, lilikuja ikiwa ni chini ya wiki moja toka mgomo wa wauza ndizi katika wilaya ya Tukuyu kuanza. Mgomo huo nao ulisababishwa na wao kupinga kuingezewa kodi katika mikungu ya ndizi ambapo mkungu mmoja ambao awali ulikuwa unaweza kuununua kwa shilingi 2500 utatakiwa ulipiwe ushuru wa shilingi 1000.

Nionavyo mimi, tatizo haliko kwenye EFDs au kiwango cha kodi ambacho kinapendekezwa kutozwa. Wala hakiko katika utunzaji wa kumbukumbu za kibiashara ili kurahisisha watu wa TRA kufanya makusanyo stahiki ya kodi. Kwa mtazamo wangu, tatizo ni "mbona viongozi na watengaji wakubwa katika mamlaka mbalimbali hususan serikalini, hawana mashine za kutunzia kumbukumbu za ahadi zao kwa wananchi?"
Ndio, ikiwa viongozi wangekuwa na mashine za kutunzia kumbukumbu za ahadi zao kwa wananchi, na kisha kukawepo na mashine (sheria) za kuwawezesha wananchi kutumia kumbukumbu hizo kuwawajibisha viongozi hao, basi hakungekuwa na malalamiko ya EFDs kwa wafanyibiashara leo hii.

Tatizo linakuja kuwa, walalahoi hawa au waganga njaa hawa, wanalazimishwa kuhakikisha wanakuwa na mashine za kutunzia kumbukumbu kwa minajili ya kuziwezesha mamlaka kuzidi kuwakamua kodi, ambazo baadae hawaoni kama zinawanufaisha kwa kiwango cha kutosha.
Muuza ndizi sokoni, analipa ushuru kila siku katika soko, analipa kodi kedekede tangia anapozinunua huko mashambani, kuzisafirisha hadi kuzipanga, lakini mahali anapoziuza, mifereji ni michafu na ili isafishwe ni lazima alipie mchango. Akitaka kwenda kujisaidia, anatakiwa kulipia pia huduma hiyo ya kwenda haja, taka zikizidi sokoni anatakiwa alipie ili zikakusanywe na kwenda kutupwa. Huyu mnapotaka kumuongezea ushuru, mnamtaka nini kama sio ubaya?

Hebu waangalie wale wafanyibiashara pale Mbeya. Analipia kodi ya pango, anapoenda kujisajili kupata namba ya mlipa kodi, anatakiwa apeleke mkataba wa upangaji sehemu yake ya biashara, na anatakiwa alipie kodi kile kiasi anachomlipa mwenye nyumba, na wala sio mwenye nyumba anayelipwa ndio alipie kipato hicho. Analipa ushuru wa eneo analofanya biashara kila siku, analipia kodi bidhaa anapozinunua, analipa kodi anapozisafirisha, analipa kodi anapozipanga tu dukani kwake. Huyu mnapotaka anunue mashine inamsaidia kwa lipi hapo?

Hivi sasa biashara nyingi sana zimekuwa zikienda kombo, ikielezwa kuwa serikali licha ya kupitisha bajeti, haijaingiza hela kwenye mzunguko, na ndio maana kwa mfano serikali hiyo inadaiwa karibu na kila aliyekuwa akiipa huduma. Hawa watu watoe wapi laki nane za kununua EFDs?

Lakini mtu huyu huyu akiumwa anajilipia matibabu, mtaa anaokaa barabara ni mbovu kupita maelezo, hakuna mitaro ya maji ya kueleweka, hakuna mifumo mizuri ya utoaji wa maji machafu. Akiumwa akienda hospitali, analazimika kwenda kununua dawa, akiumwa mwanae ndio hivyo hivyo, akiumwa baba, mama au ndugu yake yeyote hali ni hivyo hivyo. Hizi kodi za awali anazolipa zinakwenda wapi? Akinunua mashine, itamsaidia vipi kukuza biashara yake zaidi ya kuweka kumbukumbu za kuwawezesha TRA kuzidi kumkamua kodi zaidi?

Nionavyo mimi, tatizo kubwa ni kutokuwepo kwa uwiano wa kodi ambazo tayari zinakusanywa hivi sasa, na upatikanaji wa huduma katika maisha halisi. Mafanikio mengi yamekuwa kwenye hotuba ya waziri wa fedha anapowasilisha bajeti na sio katika eehemu ambazo walipa kodi wenyewe wanaishi, na hili ndio tatizo kubwa.
Ikumbukwe kuwa, mfanyibiashara ni ndugu wa mwananchi wa kawaida na mfanyakazi. Na kwamba kama huyu mwananchi wa kawaida angekuwa anaziona kodi zake na za mfanyibiashara zimemletea matunda, hakika angesimama mstari wa mbele kumshurutisha ndugu yake huyo kununua mashine kwa maslahi zaidi ya wananchi. Mfanyakazi naye pia angefanya hivyo hivyo, na mwisho wa siku, wafanyibiashara wangezinunua na kuzifanyia kazi.
Inapotokea kuwa mfanyibiashara anapogoma anaungwa mkono na kundi kubwa la walio kando ya biashara zenyewe, inamaanisha kuwa hata hawa wasio wafanyibiashara wanaona kabisa kuwa ndugu zao wanaonewa. Na bahati mbaya sana ni kuwa, mifano ya namna hii ipo haijasahaulika. Simulizi la zile mashine za kudhibiti mwendo, ziliishia wapi kama sio ajali kuzidi kuua ndugu zetu hadi leo hii? Magari yalifungiwa hadi kila moja likawa na kidhibiti mwendo, lakini leo tuko wapi?
nionavyo mimi, Watanzania tayari wanalipakodi nyingi mno, na kuwaambia eti wawe na mashine za kutunzia kumbukumbu za biashara zao, ambayo kimsingi inamaanisha mashine ya kumbukumbu za wanavyokamuliwa kodi na kubakia watupu, ni kuwataka ubaya zaidi. Kwanza viongozi watuonyeshe mashine za kutunzia kumbukumbu za ahadi zao, kisha mashine zinazowawezesha wananchi kuchukua hatua kama hawaridhishwi na utekelezaji wa ahadi walizoahidiwa awali, ndipo wafanyibiashara nao washurutishwe kumiliki mashine za EFDs.

Kama hatuwezi kuuona kwanza uwiano wa kiuhalisia wakodo ambazo tayari zinakusanywa na maendeleo ambayo tuliahidiwa, basi tutarajie kuwa hili la EFDs litakuwa moja ya mambo yatayoleta migogoro zaodo katika zama hizi ambapo wakubwa wanalazimisha kuwa zinunuliwe na wafanyibiashara.

Kama viongozi hawaoni umuhimu wa wao kuwa na mashine za kutunza kumbukumbu za ahadi zao, na kama hawaoni umuhimu wa kuktengenezea mwananchi mashine (sheria) ya kuweza kuchukua hatua dhidi ya kiongozi ambaye anamletea mambo ya kipuuzi na majibu ya ajabu ajabu pindi anapomhpomhoji, basi sioni umuhimu wa waganga njaa hawa kulazimishwa kumiliki mashine za kutunza kumbukumbu za hesabu za biashara zao. Haziwaongezei chochote katika ufanisi wa biashara zao wala ubora wa huduma za msingi.
--
Ramadhani Msangi
Founder & CEO - Jukwaa Huru Media
P. O. Box 693, Mbeya - Tanzania
Hotline: +255 767 412 176
URL: www.jukwaahuru.com