Alhamisi, 17 Oktoba 2013

KARIBU DUNIANI LEO

BURUNDI YAPATA MAKAMU WA RAIS MPYA
 
Busokoza alikuwa mfanyabiashara baada ya kustaafu kutoka katika jeshi

Nchini Burundi, Bwana Bernard Busokoza wa kabila wa watutsi na anayetoka chama cha Uprona, ameteuliwa kuwa makamu wa kwanza wa Rais wa Burundi .
Bernard Busokoza mwenye umri wa miaka 60 , anachukua nafasi ya Terence Sinunguruza aliyejiuzulu hivi karibuni baada ya kupoteza imani ya chama chake cha Uprona kwa madai kwamba alipuuza maslahi ya chama na kujiendeleza yeye binafsi.
Busokoza alikuwa afisaa wa zamani wa jeshi la zamani la Burundi baada ya kupata elimu ya kijeshi nchini Ugiriki. Hata hivyo alijihusisha na maswala ya biashara hasa katika sekta ya mawasiliano baada ya kustaafu kutoka katika jeshi.
Anamiliki mojawapo ya kampuni kubwa ya mawasiliano nchini humo.
Uteuzi huo wa Bernard Busokoza umeidhinishwa Jumatanojioni na bunge pamoja na baraza la seneti.
Hata hivyo kulikuwa na pingamizi kuhusu uteuzi wake hasa kutoka kwa wabunge wa chama cha (CNDDFDD) cha Rais Pierre Nkurunzinza wakisema kuwa aliwahi kuhusika na mapinduzi ya kijeshi yaliyosababisha kifo cha rais wa kwanza wa kihutu Milkior Ndadai
Makamu wa rais aliyemtangulia, Terence Sinunguruza alijiuzulu kutokana na shinikizo za wanachama wenzake wa (UPRONA) waliodai kuwa haonekani kutetea masilahi ya chama chake.
Chama hicho kilimtaka Rais Pierre Nkurunziza kumfuta kazi Sinunguruza, aliyetuhumiwa kwa kusababisha migawanyiko chamani tangu kuchukua wadhifa huo miaka mitatu iliyopita

WAKIMBIZI WA SYRIA WAENDELEA KUTAABIKA MISRI
Watu wengi nchini Syria wametoroka vita na kukimbilia nchi jirani

Shirika la kimataifa Amnesty International,linasema kuwa maafisa nchini Misri wanawazuilia mamia ya wakimbizi wa Syria katika mazingira mabaya sana.
Wakimbizi hao wanatoroka vita vinavyoendelea Syria.
Katika ripoti yake mpya, shirika hilo linasema kuwa idadi kubwa ya watoto wanazuiliwa wengi wakiwa hawana wazazi.
Kwa mujibu wa shirika hilo, baadhi ya wakimbizi wamezuiliwa katika vituo vya polisi ambako hali ni duni wengi wakiwa hawapati chakula wala matibabu kwa walio wagonjwa.
Linasema kuwa mjini Alexandria , mapacha wawili wenye mwaka mmoja walipatikana miongoni mwa wale waliozuiliwa.
Maafisa wa utawala bado hawajajibu tuhuma za shirika hilo.
Misri imekuwa ikikumbwa na vurugu za kisiasa tangu kuondolewa mamlakani kwa aliyekuwa Rais Hosni Mubarak mwaka 2011.

WANAJESHI WA UN WAHITAJI VIFAA ZAIDI HUKO MALI
 
NDEGE YA UN NCHINI MALI

Umoja wamataifa umeomba usaidizi wa vifaa kuwawezesha wanajeshi wake wa amani nchini Mali kushika doria.
Kikosi hicho cha UN kilianza kulinda amani nchini Mali mwezi Julai , na kina chini ya nusu ya wanajeshi 12,000 wanaohitajika kushika doria
Mjumbe maalum wa UN nchini Mali, Bert Koenders, amesema kuwa mashambulizi ya hivi karibuni yamekuwa dalili ya changamoto zinazowakumba wanajeshi hao.
Aliongeza kuwa kikosi hicho kinachojulikana kama Minusma, kinahitaji rasilimali zaidi ili kuweze kudhibiti hali Kasakazini mwa nchi.
Wanajeshi wa Ufaransaka , waliongoza operesheni dhidi ya wapiganaji wa kiisilamu na kuwaondosha kutoka katika eneo hilo.
Uchaguzi wa Urais ulifanyika mwezi Julai lakini wapiganaji hao wakaanza tena kufanya mashambulizi Kaskazini mwa nchi ambako kundi linalotaka kujitawala la Tuareg pamoja na wapiganaji wengine wamekitaka kambi.
Lakini Bert Koenders, anasema kuwa tisho la usalama linasalia kuwa changamoto kubwa.
Mshambuliaji wa kujitoa mhanga alishambulia mji wa Timbuktu tarehe 28 Septemba huku wapiganaji wa kiisilamu nao wakilipiza mashambulizi hayo kwa kurusha makombora.
Kikosi cha kulinda amani cha UN kilipata pigo jengine mwezi Agosti baada ya idadi nyengine kubwa ya wanajeshi wa Nigeria kurejea nyumbani kupambana na wanamgambo wa Boko Haram.
Hatua hii iliwaacha wanajeshi wa UN na chini ya wanajeshi elfu sita. Idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi wanajeshi 12,640 ifikapo mwezi Disemba.
UN inatarajiwa kuwapeleka wanajeshi wengine huko kuchukua nafasi ya wanajeshi wa Ufaransa waliorejea nyumbani baada ya kuingilia kati mgogoro huo wapiganaji walipotishia kuvamia mji mkuu wa Mali Bamako mwezi Januari.
Wapiganaji hao wenye uhusiano na kundi la kigaidi la Al Qaeeda walidhibiti Kaskazini mwa Mali, ikiwemo miji mingine mikubwa ya Gao, Kidal na Timbuktu, baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika mwezi Machi mwaka 2012.

 

Hakuna maoni: