Ijumaa, 11 Oktoba 2013

NINI KINAENDELEA BAADA YA KIFUNGO CHA SIKU 14?



 Wasomaji wa Gazeti la Mwananchi leo wanaanza kupata uhondo wa habari baada ya wiki mbili za kufungiwa
Uongozi wa Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL), umetangaza kurejea kwa Gazeti la Mwananchi mitaani na kuushukuru umma kwa kuwa nao bega kwa bega katika kipindi lilipofungiwa na Serikali.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mkurugenzi Mtendaji wa MCL, Tido Mhando alisema kwa mujibu wa agizo la Serikali la kutochapishwa kwa Gazeti la Mwananchi, adhabu ilimalizika jana.
Mhando alisema kuanzia leo gazeti litakuwa mitaani kama kawaida na kuwaahidi wasomaji kuwa wataendelea kupata gazeti lenye habari za uhakika zinazojikita kwenye umahiri, uhuru, weledi wa uandishi na uhariri.

UNAJUA TUZO YA NOBEL MWAKA HUU IMECHUKULIWA NA NANI NA WAPI?


Wakaguzi wa silaha za kemikali Syria

Tuzo ya amani ya Nobel, mwaka huu imekwenda kwa shirika la kudhibiti silaha za kemikali duniani OPCW.
Shirika hilo kwa sasa linasimamia shughuli ya kuharibu silaha za kemikali za Syria ambazi zilitumiwa kwa mauaji ya raia wa nchi hiyo mjini Damascus mwezi Agosti.
Tangazo hili limetolewa mjini Oslo, Norway.
Kufuatia uamuzi huu, kamati ya Nobel nchini Norway imetambua kazi ya shirika hilo ambalo linaendesha shughuli ya kuharibu silaha za kemikali, kama sehemu ya azimio la kimataofa la kuharibu silaha za kemikali ambalo limesemekana kufanikiwa sana duniani.
Shirika hilo la kuzuia matumizi ya silaha za kemikali , pia husimamia azimio la silaha za kemikali duniani ambalo limefanikiwa kuharibu asimilia 80 ya zana za kemikali duniani.
Syria inatarajiwa kuwa nchi ya 131 kutia saini azimio hilo.
Nchi hiyo inasemekana kuwa na idadi kubwa ya silaha za kemikali duniani.
Tuzo ya leo kwa OPCW itaonekana kama hatua ya kutia moyo kwa shirika hilo kuendelea na kusaidia katika kutatua mgogoro wa kisiasa unaoendelea Syria
Waakilishi wa shirika hilo wataalikwa kupokea medali na tuzo ya dola milioni 1.2 za kimarekani wakati wa sherehe zitakazofanyika mwezi Disemba.


MSIKIE ZITTO KABWE KATIKA KAULI YAKE JUU YA SIASA

Zitto: Natafakari upya uamuzi wangu
NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Zitto Kabwe, amesema anatafakari upya uamuzi wake wa kuachana na siasa baada ya kushuhudia hali ngumu ya maisha inayowakabili wananchi wa mkoa wa Tabora.
Alisema kutokana na hali duni ya maisha ya wananchi aliyoishuhudia katika maeneo mbalimbali kwenye majimbo ya Sikonge na Igalula, atahakikisha kwa kushirikiana na viongozi wenzake ndani ya CHADEMA wanakifuta Chama cha Mapinduzi (CCM) katika Kanda ya Magharibi.
Zitto ambaye alikwishakutangaza kutogombea tena ubunge katika Jimbo lake la Kigoma Kaskazini kwenye Uchaguzi Mkuu ujao, alitoa kauli hiyo juzi katika mikutano ya hadhara, katika majimbo ya Sikonge na Igalula, ukiwa ni mwendelezo wa ziara yake ya ujenzi wa chama katika kanda hiyo.
Maeneo aliyoyatembelea na kukuta hali ya wananchi ikiwa hairidhishi hususan katika kupata huduma ya maji ni kata za Ipole, Kitunda na Sikonge, zilizo jimboni Sikonge na kata za Miswaki, Kigwa na Loya zilizoko Igalula, wilayani Uyui.
Alisema kuwa licha ya wabunge wa mkoa huo kutokana na chama kinachotawala kwa zaidi ya miaka 50, wamekosa sauti ya kuzungumzia matatizo ya wananchi kwa sababu ya kulinda masilahi binafsi.
Zitto alifafanua kuwa ni jambo la kusikitisha kuona mikoa ya magharibi ikiwa nyuma kimaendeleo licha ya kuchangia kiasi kikubwa cha fedha za kigeni katika pato la taifa kupitia kilimo cha tumbaku.
“Ninatafakari upya uamuzi wangu wa kuachana na siasa, ni vigumu kama sitashirikiana na wenzangu kuhakikisha hali hii ya watu kugombea maji ya kunywa na wanyama katika shimo moja inakwisha,” alisema.
Aliwataka wananchi wawaunge mkono pale wanapopambana bungeni hata ikibidi kupanda juu ya meza au kutoka nje pindi masilahi ya watu yanapopuuzwa, kwa sababu ya kuwapo kwa wabunge wengi wa CCM ndani ya Bunge.
Zitto aliongeza kuwa serikali ya CCM imechoka na haiwezi kuongoza na kwamba kama ilishindwa kusimamia reli iliyojengwa na wakoloni haiwezi kuongoza nchi iliyogubikwa na umaskini licha ya kuwa na utajiri kila sehemu.
“Laiti kama mngejua yale tunayoyajua na kuyapigania bungeni hususan ufisadi unaofanywa na serikali ya CCM, naamini wananchi mngeingia barabarani kuhakikisha serikali hii inatoka madarakani,” alisisitiza.
Akizungumzia uamuzi wa Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi wa vyama vya CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi kujadili muswada wa sheria wa Katiba, Zitto alisema ni wazi amedhihirisha kwamba Waziri Stephen Wassira alikuwa akiongea kitu ambacho hakijui.
Alisema wakati wapinzani walipotoka bungeni kupinga muswada huo, Wassira alisimama hadharani na kusema kwamba wapinzani hawatapata fursa nyingine ya kujadiliana na Ikulu kuhusu Katiba.
Akiwa katika Kata ya Loya, Jimbo la Igalula, Zitto alisema kitendo cha serikali kuwanyanyasa wafugaji ni udhalilishaji dhidi ya utu, kwa kuwa kila Mtanzania ana haki ya kuishi sehemu yoyote ili mradi asivunje sheria.
Alisema viongozi wa CCM wamekuwa wakiwatumia wafugaji kama mifuko yao ya hifadhi, kwa kujipatia fedha kinyume cha sheria, hali aliyoelezea kuwa ni ukiukaji wa utawala bora.
Zitto alieleza kusikitishwa na taarifa ya walimu wa Kata ya Loya kuwa wanatumia sh 20,000 kwa ajili ya kuweza kufika barabara kuu ya kuelekea mjini Tabora kufuatilia mishahara yao.

CHANZO NA TANZANIA DAIMA

GOODMORNING MTANZANIA MWENZANGU

AU KUJADILI UHUSIANO WAKE NA ICC

AU inajadili swala hili baada ya ICC kupuuza ombi la kutaka kuhamisha kesi za Kenyatta na Ruto
Marais wa Afrika wanakutana wikendi hii mjini Addis Ababa nchini Ethiopia kujadili uhusiano wa bara la Afrika na mahakama ya kimataifa ya jinai ICC.
Mkutano huu maalum umeitishwa baada ya ICC kukataa ombi la wanachama 54 wa Muungano wa Afrika kurejesha kesi za Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto nyumbani.
Viongozi hao wanatarajiwa kujadili hoja ya kujiondoa kutoka kwa mahakama hiyo.
Baada ya miezi kadhaa ya kutofautiana kati ya ICC na AU, viongozi wa Afrika wanakutana katika makao makuu ya AU katika kile kinachosemekana ni kutafakari upya uhusiano wa bara hilo na mahakama ya ICC.
Kwa mujibu wa AU, mahakama hiyo ya ICC imekosa kushughulikia ombi lililowasilishwa na AU mwezi Mei kuhusu kesi za Kenya. AU inasema kuwa ICC ina njama za kibaguzi dhidi ya viongozi wa kiafrika.
Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto wanakabiliwa na kesi za ukiukwaji wa haki za binadamu katika mahakama hiyo.
Kesi yao inahusiana na ghasia za baada ya uchaguzi mkuu Kenya mwaka 2007/2008 ambapo zaidi ya watu 1100 waliuawa.
Hata hivyo viongozi hao wamekanusha madai hayo.
Bunge la Kenya ambalo lina idadi kubwa ya wabunge wa mrengo wa Jubilee unaotawala nchi, tayari lieanzisha hoja ya kuondoa Kenya kutoka katika mahakama ya ICC.
Lakini serikali ya Kenya imesema haijashinikiza nchi za Afrika kujadili hoja ya kujiondoa ICC licha ya kuungwa mkono na majirani zake kama Uganda na Rwanda.
Naibu mwenyekiti wa AU Erastus Mwencha, ameambia BBC kuwa swala hilo sasa ni zaidi ya kutaka tu kujiondoa ICC.
Wadadisi hata hivyo wanasema kuwa huenda AU isikubali kwa ujumla kujiondoa ICC. Baadhi ya nchi kama Ghana na Botswana tayari zimepinga hatua ya kujiondoa ICC.




WABAKAJI WAADHIBIWA KWA KUKATA NYASI KENYA


Mwathiriwa alisema kuwa anawajua wabakaji

Wakenya wameghadhabishwa sana na hatua ya wanaume watatu waliombaka msichana mmoja na kutupa mwili wake kwenye choo kuamrishwa na polisi kukata nyasi kama adhabu kwao.
Msichana huyo alishambuliwa na kubakwa akiwa njiani kutoka kwa mazishi ya babu yake katika kijiji kimoja Magharibi mwa nchi.
Kwa mujibu wa taarifa za gazeti la Daily Nation nchini Kenya, uti wa mgongo wa msichana huyo ulivunjika wakati wa ubakaji na sasa amelazimika kutumia kiti cha magurudumu.
Wanaharakati wa kutetea haki za binadamu pamoja na wabunge wamelaani polisi kwa kukosa kuchunguza madai ya msichana huyo.
Msichana huyo alinukuliwa akisema kuwa anataka waliomfanyia kitendo hicho kukamatwa na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.
Idara ya polisi inawachunguza polisi waliopokea malalamishi ya msichana huyo , alisema Halima Mohammed , kamanda wa polisi katika jimbo la Busia ambako kitendo hicho kilitokea.
Hii bila shaka inaonyesha wazi ulegevu wa polisi katika kukabiliana na vitendo kama hivi na ambao wakenya wanahisi kuwa unakumba idara ya polisi , hasa baada ya mashambulizi ya kigaidi nchini humo wiki mbili zilizopita.
Msichana huyo aliwafahamu vyema waliombaka na polisi walirekodi kesi dhidi ya watatu hao.
Wanakijiji waliwapeleka watatu hao kwa polisi baada ya kusikia taarifa za kitendo hicho.
Lakini waliamrishwa kukata nyasi katika bustani la makao ya polisi na kisha baadaye kuachiliwa, alisema mamake mwathiriwa.
Masaibu ya msichana huyo yalijadiliwa na kamati ya bunge kuhusu usalama na kusema kuwa kitendo hicho ni cha kushutua sana na lazima wakifanyie uchunguzi.
Kwa mujibu wa Bi Mohammed, mama ya msichana huyo aliamrishwa kumsafisha mwanawe ili ushahidi wowote dhidi ya washukiwa uweze kupotea.
Msichana huyo sasa amelemazwa na kulazimishwa kutumia kiti cha mgurudumu.