Ijumaa, 1 Novemba 2013

LIGI KUU TANZANIA BARA YAINGIA DOSARI NI BAADA YA MASHABIKI WA SIMBA KULETA VURUGU UWANJANI

 
Kikosi cha Klabu ya Simba ya Tanzania

Polisi jijini Dar es Salaam Tanzania wamelazimika kutumia Mabomu ya machozi kuwatawanya mashabiki wa Klabu ya Simba,baada ya kumalizika mechi ya Ligi kuu soka Tanzania bara siku ya Alhamis ambapo Simba ilitoka sare ya kufungana bao 1-1 na timu ya Kagera Sugar.
Vurugu hizo zimezuka mwishoni mwa mechi ambayo timu ya Simba imezidi kuporomoka hadi nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi hiyo kufuatia matokeo ya sare ya bao 1-1.
Baada ya Simba kuongoza bao 1 hadi dakika ya 90 Kagera Sugar waliposawazisha kwa Penati iliyotiwa kimiani na beki wa zamani wa Simba Salum Kanoni ambapo mashabiki wanaoaminika kuwa wa Simba walianza kung'oa viti uwanjani hali iliyosababisha askari polisi kurusha mabomu ya machozi ili kuwatawanya mashabiki hao.
Simba ilianza kuliona lango la Kagera Sugar katika dakika ya 45 baada ya mshambuliaji raia wa Burundi Amis Tambwe kufunga bao la kwanza lililodumu hadi mapumziko.
Katika Kipindi cha pili Simba walianza kucheza kwa kujihami hali iliyosababishga Kagera kukaribia lango lao mara kwa mara na hatimaye wakafanikiwa kusawazisha katika dakika ya 90.
Kwa matokeo hayo Simba imeporomoka hadi nafasi ya nne wakiwa na pointi 21,huku Azam, wakishika nafasi ya kwanza kwa kuwa na pointi 23 sawa na Mbeya City lakini wakitofautiana kwa magoli ya kufunga.
Yanga ni ya tatu kwa kuwa na pointi 22.

UHABA WA CHAKULA KWENYE KAMBI ZA WAKIMBIZI HURUMA

DADAAB NA KAKUMA ZAKUMBWA KWA KIASI KIKUBWA
 
Dadaab ndio kambi kubwa zaidi ya wakimbizi duniani 

Shirika la chakula duniani WFP pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi (NHCR) yametangaza kuwa kuanzia tarehe moja mwezi Novemba, shirika la WFP litalazimika kupunguza kiwango cha chakula ambacho kinatolewa kwa wakimbizi zaidi ya nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Dadaab na Kakuma.
Hali hii kwa mujibu wa mashirika hayo inatokana na WFP kukosa rasilimali za kutosha kuendesha shughuli zake za kuwalisha wakimbizi katika kambi hizo.
"tumefanya kila tuwezalo kujaribu kuzuia hili , lakini imetulazimisha kupunguza kiwango cha chakula tunachotoa kwa wakimbizi hao kwa asilimia 20, kuanzia mwezi Novemba na Disemba ili tuweze kuhakikisha hifadhi yetu ya chakula itatumika hadi mwishoni mwa mwaka,’’ shirika la habari la Reuters lilimnukuu Ronald Sibanda mkuu wa shirika la WFP nchini Kenya.
"Tunatumai kuwa hali hii itakuwa tu ya muda huku tukiwaomba wahisani wetu kuja kuwasaidia mamia ya wakimbizi wanaotegemea msaada wa chakula wa WPF ili kukimu mahijati yao,’’ aliongeza kusema bwana Sibanda.
Shirika hilo linahitaji dola milioni kumi kila mwezi ili kutoa chakula karibu tani elfu kumi kwa wakimbizi katika kambi hizo mbili zilizoko Kaskazini mwa Kenya.
Hata hivyo chakula kilichoko sasa kinaweza kutosheleza wakimbizi 535,000 walio kwenye kambi hadi mwishoni mwa mwaka na huenda wakapunguza chakula hicho zaidi ikiwa shirika hilo halitapata msaada zaidi.
Bwana Sibanda amesema kuwa anaamini jamii ya kimataifa inaelewa umuhimu wa mpango wao kuwasaidia wakimbizi katika kambi za Dadaab na Kakuma na kwamba wana wasiwasi kuwa kupuguka kwa msaada wa chakula kwa wakimbizi ni jambo litakalokuwa na atahri kubwa sana.
Mpango wa WFP kuwasaidia wakimbizi nchini Kenya umekumbwa na changamoto nyingi katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Mchango wa Marekani wa dola milioni ishirini unatarajiwa kutolewa mwezi Machi mwaka 2014 lakini shirika hilo litahitaji dola milioni ishirini kuendelea na shughuli zake kati ya mwezi Januari na Februari kuhakikisha kuwa wakimbizi wanapata lishe bora na chakula kwa ujumla kwani wengi wao hawana chanzo kingine cha chakula.