Jumanne, 8 Oktoba 2013

HII SIYO TANZANIA TU..:MAANDAMANO YA WALIMU BRAZIL YAZUA GHASIA


Walimu wamekuwa wakidai mishahara bora kwa muda mrefu

Maandamano ya watu waliokuwa wanaunga mkono walimu wanaodai mishahara bora zaidi nchini Brazil, yamegeuka na kuwa makabiliano kati yao na polisi katika miji ya Rio de Janeiro na Sao Paulo.

Mji wa Rio ulikuwa umesongamana watu zaidi ya 10,000 wakiandamana kwa amani .
Lakini usiku ulipoingia, waandamanaji kadhaa walirusha mabomu ya moto katika majengo ya serikali nao polisi wakawarushia gesi ya kutoa machozi ili kuwatawanya.

Maandamano sawa na hayo yalitokea mjini Sao Paulo na pia kusababisha ghasia na makabiliano makali kati ya polisi na waandamanaji hao waliokuwa wamefunika nyuso zao na kuvamia benki.
Hali ya usalama nchini Brazil, ni changamoto kubwa ambayo huenda ikajitokeza zaidi wakati wa kombe la dunia mwaka 2014 na michezo ya olimpiki mwaka 2016 .

Maandamano ya hivi karibuni yalidumu kwa masaa kadhaa na yalikuwa salama mwanzoni.
Lakini usiku ulipoingia ghasia zikazuka huku waamdanamanaji wakiteketeza majengo ya serikali na wengine kuvamia benki na kuvunja mashine za pesa. Baadhi ya benki ziliteketezwa.

Waandamanaji hao pia waliiba viti kwenye benki na kuvitumia kama vizuizi kati yao na polisi.
Polisi walilazimika kutumia gesi ya kutoa machozu kurejesha utulivu.Walimu wamekuwa wakidai nyongeza ya mishahara kwa miezi kadhaa sasa. 

Takriban watu 50,000 walikadiriwa kuandamana ili kuwaunga mkono walimu kabla ya ghasia kuzuka lakini polisi waliweza tu kuthibitisha watu 10,000 walishiriki maandamano hayo.

Hakuna maoni: