Jumamosi, 7 Septemba 2013

Wanafunzi albino watelekezwa shuleni Bughangija


 Wanafunzi Albino wakiwa wamepumzika nje ya eneo la shule.

Shinyanga. Shule ya Msingi Maalumu Buhangija iliyopo Manispaa ya Shinyanga ililenga kuwasaidia watoto wasioona.
Lakini kutokana na kuzuka kwa wimbi la mauaji ya walemavu wa ngozi (albino), mwaka 2009 shule hiyo iliamua kuwahifadhi hapo ili kulinda usalama wao pamoja na kuwapatia elimu.
Shule hiyo kwa sasa inalea watoto mchanganyiko wakiwemo wasiiona 37, viziwi 46 na walemavu wa ngozi (albino) 164, ambapo licha ya kuwa chini ya Serikali kupitia halmashauri husika, kwa kiasi kikubwa inategemea msaada kutoka kwa wafadhili ambao ni mashirika, wahisani pamoja na watu binafsi kutokana na Serikali kuitelekeza.
Watoto wanaosoma Buhangija Maalumu, wamekuwa wakiishi kwa dhiki kubwa kutokana na uhaba wa fedha za kuwahudumia, mahitaji muhimu kama vile chakula, malazi
na matibabu hali ambayo huwafanya kushinda njaa au kupata mlo mmoja kwa siku au pengine kushindia uji.
Katika mahojiano na gazeti hili, mwalimu mkuu wa shule hiyo Peter Ajali, anasema kuwa watoto hao wapo chini ya Serikali kupitia halmashauri husika iliyoelekezwa kuwa kila mtoto alipiwe Sh2,500 kwa siku, ikiwa ni gharama ya chakula, matibabu pamoja na makazi bora, lakini bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na mzigo huo kuegemea Manispaa ya Shinyanga pekee.
Mwalimu huyo anasema kuwa halmshauri zote za Mikoa ya Shinyanga, Simiyu pamoja na Geita ambazo zina watoto shuleni hapo zilitakiwa kutoa kiasi hicho cha fedha, lakini zimekuwa hazifanyi hivyo jambo linalosababisha kuwa na deni la zaidi ya Sh180 milioni hadi sasa.
“Hapa shuleni kuna walemavu wa ngozi kutoka wilaya za Mikoa ya Shinyanga, Simiyu pamoja Geita, hivyo kila wilaya inawajibika kwa watoto wake kwa kuwalipia Sh2,500 kwa siku, lakini cha kusikitisha ni kuwa mzigo huo umeachiwa Halmashauri ya Manispaa hii (Shinyanga) na ndiyo sababu matatizo haya hayatatuliki,” anasema Mwalimu Ajali.
Anatolea mfano kuwa mwezi Machi mwaka huu, Serikali ilituma Sh19 milioni ikiwa ni bajeti ya miezi mine, ambayo ni sawa na Sh6 milioni kwa kila mwezi, huku bajeti ya chakula pekee shuleni hapo kwa mwezi ikiwa ni zaidi ya Sh13, tofauti na gharama nyingine kama vile maji, umeme na matibabu .
Kuhusu wazazi wao
“Kwa kweli uendeshaji wa shule hii ni kazi ngumu, kwani wakati mwingine tunalazimika kukopa madukani ili watoto hawa wasilale njaa, kwani kula mlo mmoja au kushindia uji ni jambo la kawaida shuleni hapa,” anaeleza Mwalimu Ajali.
Akizungumzia upande wa walemavu wa ngozi mwalimu huyo anasema kuwa wengi wanafunzi hao wametelekezwa na wazazi wao kwani tangu walipofikishwa kituoni hapo, wazazi hawajawahi kurudi kufuatilia maendeleo ya watoto wao kielimu wala kiafya, jambo ambalo linaongeza mzigo kwa shule hiyo kutokana na kukosa ushirikiano kutoka kwa wazazi husika.
“Iwapo wazazi wangekuwa wanakuja mara kwa mara, huenda hili tatizo lingepungua kwani nina imani wangewasaidia mambo machache kama mavazi na matibabu. Lakini ni asilimia 6 hadi 25 pekee hufika shuleni hapo kwa mwaka, tena mara moja kuwaangalia watoto wao, huku asilimia 75 wakiwa hawafiki kabisa,”analalamika Ajali.
Kutokana na hali hiyo mwalimu mkuu huyo anasema kuwa hajui hatima ya watoto hao watakapomaliza shule kwani hata wakati wa likizo huwa hawaendi nyumbani kwa kuhofia usalama wao, huku wengine wakiwa hawafahamu makwao kutokana na kuletwa shuleni hapo wakiwa na umri mdogo wa miaka mitano huku wazazi wao wakiwatelekeza moja kwa moja.
Ajali anasema kuwa, pia shule hiyo inakabiliwa na uhaba wa mabweni kwa wasichana na wavulana akieleza kwamba mabweni yaliyopo yana uwezo wa kukaa watoto 100, lakini kwa sasa yana watoto 247.
Anaeleza kuwa kutokana na changamoto hiyo, watoto hao wanalazimika kulala wanne katika kitanda kimoja, badala ya watoto wawili, ongezeko ambalo ni sawa na asilimia 147.
Hata hivyo, anasema kuwa Serikali pia imeshindwa kuwahudumia walemavu hao kwa kuwapatia mafuta maalumu ya kuwakinga na mionzi ya jua, jambo ambalo linawaleka katika mazingira na wakati mgumu kwani ngozi zao zinaathiriwa zaidi na mionzi ya jua.
Akizungumzia elimu Mwalimu Ajali alisema kuwa, kitaaluma watoto hao wanaonyesha jitihada kubwa huku wengi wao wakisomeshwa kwa ufadhili wa Shirika la Under The Same Sun (UTSS) la nchini Canada, ambalo hadi sasa linasomesha watoto 51 elimu ya msingi na sekondari, ambapo lengo kuwasomesha hadi chuo kikuu.
Kwa upande mwingine anasema kuwa kituo hicho kinakabiliwa na uhaba wa walezi na kwamba waliopo hawakidhi mahitaji, huku walezi wakiwa 12 na wanane kati yao, wameajiriwa na UTSS, wanne wameajiriwa na Serikali, huku mahitaji halisi ni kuwa na walezi 20.
Asemavyo DC
“Pia kuna tatizo la madai ya wapishi na walinzi kwani wana muda mrefu, zaidi ya miezi saba hawajalipwa mishahara yao. Kwa kweli inasikitisha kuona mtu anafanya kazi muda wote huo lakini halipwi, kwa upande mwingine naweza kusema wana moyo wa pekee kwani bado wanafanya kazi kwa moyo mmoja,” anasema.
Hata hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Annarose Nyamubi akiwa shuleni hapo hivi karibuni anawataka wazazi na walezi wa watoto hao kujenga tabia ya kuwatembelea mara kwa mara ikiwa ni pamoja na kuwachukua wakati wa likizo ili kuwa karibu na familia zao.
Nyamubi aliyasema hayo baada ya kupokea taarifa kutoka kwa mwalimu mkuu wa shule hiyo iliyoeleza kwamba wengi wa wazazi na walezi wamewatelekeza watoto wao, huhu mkuu huyo wa wilaya akisisitiza kuwataka wazazi kuwa karibu na watoto wao akiwahakikishia ulinzi na usalama wao wawapo nyumbani wakati wa likizo.
Wanafunzi wanasemaje?
Kwa upande wao wanafunzi hao (walemavu wa ngozi) wanasema kuwa licha kukumbana na changamoto nyingi shuleni hapo zikiwemo uhaba wa chakula, mabweni, matibabu, mafuta maalumu ya kujikinga ya mionzi ya jua pamoja na vifaa vya kujifunzia, wamekuwa wakiendelea kuishi shuleni hapo hata baada ya likizo kwa kuhofia usalama wao wawapo nyumbani kwao.
Semeni Deus (13) mwanafunzi wa darasa la sita anasema kuwa alitokea Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu mwaka 2010 kutokana na kushamiri kwa mauaji ya albino na kwamba amekuwa akiishi shuleni hapo siku zote hata wakati wa likizo huku wazazi wake wakija kumsalimia.
“Mimi nimetoka Wilaya ya Kahama tangu mwaka 2009, lakini tangu nimekuja hapa sijawahi kurudi nyumbani kutokana na kuhofia usalama wangu. Ila tuna shida sana hapa shuleni kama vile chakula kwani hakitoshi hali inayosababisha wakati wa kula kunyang’anyana. Pia kuna tatizo la malazi, bwenini tumebanana sana, matibabu pamoja na mavazi na mafuta ya kujikinga na mionzi ya jua, ” anasema Hassan Khamis mwanafunzi wa kidato cha pili.
Wanaiomba Serikali iwasaidie wakieleza kuwa wanaishi kwa dhiki kubwa na kwamba hawana pa kukimbilia zaidi ya kuitegemea Serikali ambayo imewasaidia kulinda usalama wao hadi sasa shuleni hapo.
 

Hakuna maoni: