UKITAKA KUUNGANISHA UMEME TANZANIA JIANDAE KISAIKOLOJIA
Ukitaka kuunganishiwa umeme nchini Tanzania ni lazima uache kazi
ufanye kazi ya kuunganishiwa huduma hiyo. Hii inatokana na ukweli
kwamba kama unataka umeme, huna budi kuacha unachofanya na kutumia muda
mwingi kukamilisha huduma hiyo tena kwa gharama kubwa.
Watu wengi wanashauri ni vyema kama unataka huduma
ya umeme ukajiandaa kisaikolojia kwa kuwa itakulazimu kutumia fedha
nyingi na muda mwingi kupata huduma hiyo.
Kutokana na mazingira hayo, uanzishaji wa biashara
kubwa na hata zile ndogo zinazohitaji nishati, wahusika wanalazimika
kusubiri huduma ya umeme.
Siku 109 kupata umeme
Kwa mujibu wa ripoti iliyomo katika taarifa ya
kufanya biashara ya Benki ya Dunia ya ‘The World Bank’s Doing Business’
ya mwaka huu ambayo iliangalia nchi 185 duniani, ilibaini kwamba
inachukua siku 109 na gharama ya asilimia 1,944.1 ya pato la mtu kwa
mwaka nchini Tanzania kukamilisha mchakato wa kuunganishiwa umeme.
Pia taarifa hiyo ilibainisha kwamba kuna mambo
manne ambayo lazima yafuatwe ili mfanyabiashara kupata ghala
lililounganishwa na umeme kwenye maeneo ya kibiashara ndani ya jiji.
Mambo hayo manne yanayopaswa kufuatwa ni; kupeleka
maombi kwa kampuni ya ugavi wa umeme ya Shirika la Umeme Tanzania
(Tanesco) na inakuchukua siku 11 kupata majibu ya maombi yako.
Fundi umeme aliyesajiliwa anapaswa kuwasilisha
hati inayoonesha kazi ya kuweka nyaya za umeme katika eneo husika,
imefanyika kwa mujibu wa kanuni na kwa viwango vinavyotakiwa.
Baada ya hapo mteja ananunua transfoma ili kufanya
shughuli za maunganisho nje na kazi hiyo inachukua miezi mitatu. Jumla
ya gharama zinazotumika hapa ni Sh16 milioni.
Pia kuna fedha zitakazotumika kwa ajili ya kulipia
gharama za maunganisho na za dhamana na wakati mwingine mteja
analazimika kununua baadhi ya vifaa muhimu vya kuwezesha maunganisho
nje.
Muda mrefu unaotumika na vikwazo vinavyojitokeza
katika mchakato wa kuingiza umeme katika ghala au sehemu ya biashara
imesababisha Tanzania kuwekwa katika nafasi mbaya ya 96 kati ya nchi 185
duniani endapo mtu anahitaji huduma ya kuunganishiwa umeme.
Nafasi ya hiyo kwa Tanzania inatisha kwa kuwa
inaonyesha ni jinsi gani wawekezaji wanatumia muda mwingi kutafuta
kuunganishiwa umeme huku wengine wakilazimika kutumia majenereta wakati
wakisubiri umeme na kuongeza gharama za uzalishaji.
Baadhi ya viwanda vya saruji jijini Dar es salaam havijaanza kufanyakazi kwa sababu havijaunganishiwa umeme,” anasema Mkurugenzi wa sera na utetezi wa Shirikisho la Viwanda nchini (CTI), Hussein Kamote.
Baadhi ya viwanda vya saruji jijini Dar es salaam havijaanza kufanyakazi kwa sababu havijaunganishiwa umeme,” anasema Mkurugenzi wa sera na utetezi wa Shirikisho la Viwanda nchini (CTI), Hussein Kamote.
Mkurugenzi huyo anaitaka Tanesco kuondokana na vikwazo vinavyochelewesha maunganisho ya umeme ili kuvutia wawekezaji nchini.
“Hatujafanya utafiti kuhusu upatikanaji wa umeme
nchini, lakini tunaamini kwamba ni eneo linalotakiwa kuangaliwa kwa
makini,”anasema Kamote.
Kwa mujibu wa ripoti ya Benki ya Dunia, mchakato
wa kuunganisha umeme nchini unakuwa mgumu kutokana na sheria na kanuni
kadhaa zinazotakiwa kufuatwa kugusa; ubora, usalama, masuala ya
kiufundi, ununuzi ni suala la utandazaji wa nyanya ndani ya ghala.
Kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na Shirikisho la
wenye Viwanda nchini (CTI ) kwa ufadhili wa Best Ac, mwaka 2011
umeonyesha kwamba kuna matatizo mengi yanayokumba sekta ya nishati
nchini Tanzania.
Kwa kukabiliana na tatizo hilo utafiti huo
ulishauri Tanesco kugawanya kampuni na kuwa mbili. Kampuni moja kwa
ajili ya kufua umeme na kampuni ya pili kwa ajili ua kusambaza umeme.
Kwa mujibu wa utafiti huo, kampuni mbili
zitasaidia wateja wa umeme kupata unafuu wa kupata huduma kwa mfano,
kuunganishiwa umeme na kulipia huduma ya akra za umeme.
Vilevile kuwapo kwa kampuni mbili, kutachangia
kuwa na kasi katika maunganisho ya umeme na kuboresha ukuaji wa kampuni
ya Tanesco hasa kutanua wigo wake.
Uwezo huo wa kutanua wigo umedhihirishwa pia
katika utafiti uliofanywa wa ‘Provision of Financial Advisory and
Modelling Services to Tanesco: Cost of Service’ uliofanywa mwaka 2010,
ambao ulibainisha kuwa Tanzania ina kiwango kidogo cha kasi ya
uunganishaji umeme na kwa mwaka 2008 ilikuwa ni asilimia 14 wakati idadi
ya watu ikiwa ni 42milioni.
Uwapo wa watu wengi kiasi hicho unaweza kuwa
nafasi nzuri ya kutanua soko la Tanesco na wanaweza kuingiza wateja
wapya 100,000 kila mwaka na kutoa nafasi zaidi ya ukuaji. Hali hiyo
haijafikiwa mpakasa sasa.
Kwenye mkutano wa mashirika ya nishati ,
uliofanyika Februari hadi Machi mwaka huu mjini Washington DC,
Marekani ilibainisha kwamba Tanesco ina uwezo wa kuunganisha wateja
wapya 90,000.
Januari mwaka huu serikali ilifanya mabadiliko
katika gharama hizo na kwa watu walio umbali wa mita 30 kutoka katika
laini ya umeme na kuhitaji nguzo moja gharama yake ilipungua kwa
asilimia 60 mpaka asilimia 75.
Gharama zimepungua
Kwa wakazi wa mjini gharama za maunganisho
zilipungua kwa asilimia 29 mpaka asilimia 60 na kwa Mkoa wa Lindi na
Mtwara, wakazi wa huko watatozwa dola 62 za Marekani kwa umeme wa
majumbani na viwandani.
Tanesco katika mpango kazi wake ilifanya uamuzi wa
kufanya maunganisho 250,000 kwa mwaka kutoka katika gridi ya taifa na
kuongeza idadi ya watu wanaopata umeme kutoka asilimia 14 hadi 30
ifikapo mwaka 2015.
Ingawa kuna shida hiyo ya umeme taarifa ya mwaka
huu ya Doing Business, Tanzania ilifanya vyema zaidi kuliko Kenya
iliyoshika nafasi ya 162, Uganda nafasi ya 127, Msumbiji nafasi ya 174
na Malawi iliyokuwa ya 176. Hata hivyo Tanzania ilifanya vibaya katika
baadhi ya maeneo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni