Jumatatu, 7 Oktoba 2013

GOODMORNING TANZANIA


HATUA ya Serikali ya Tanzania kuyafungia magazeti mawili ya kila siku, Mtanzania (kwa siku 90) na Mwananchi (siku 14), imesababisha mjadala wa hali ya juu katika maeneo mbalimbali barani Afrika.


Gazeti la Mail&Guardian la Afrika Kusini, liliandika kuwa hatua hiyo ni kusambaratisha uhuru wa vyombo vya habari na kuwanyima wananchi haki ya kupata habari. 

Gazeti hilo liliendelea kudai kuwa hatua ya kufungia vyombo vya habari ni kuvunja maana ya upashanaji habari, ambayo inatakiwa kuwafikia wananchi. 

Chombo hicho cha habari kimeifananisha adhabu hiyo ya kuyafungia magazeti hayo mawili kama ile iliyochukuliwa na Serikali ya Uganda, mwanzoni mwa mwaka huu ya kulifungia gazeti jingine la NMG, la Daily Monitor, kwa madai lilichapisha habari ya uchochezi.

Tangazo la Serikali ya Tanzania kupitia Gazeti la Serikali namba 333 Septemba 27 mwaka huu lilitangaza magazeti ya Mwananchi na Mtanzania yamefungiwa.

Katika hatua nyingine, gazeti la Mail&Guardian lilimkariri Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, akisema kuwa “Kufungia magazeti hakutazuia haki ya wananchi kutoa maoni yao na kupambana mpaka kupatikana utawala bora. 

“Kwanza kufungiwa kwa magazeti hayo kutawaimarisha waandishi kwa kiwango cha juu. Unalifungia gazeti kwa kutoa taarifa za mishahara? Tatizo liko wapi, je, watu hawatakiwi kujua mishahara ya watumishi wa umma?”

Ikitumia Sheria ya Magazeti ya Mwaka 1976, Serikali kupitia kwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Assah Mwambene, iliyafungia magazeti hayo kwa madai ya kuchapisha habari zenye mwelekeo wa uchochezi na uvunjifu wa amani. Serikali ilitangaza kulifungia Mwananchi kwa siku 14 na Mtanzania siku 90, kuaNzia Septemba 27, mwaka huu. 


Uamuzi huo ulichukuliwa na serikali kwa madai kwamba, magazeti hayo yaliandika habari na makala za uchochezi na uhasama kwa nia ya kusababisha wananchi wakose imani kwa vyombo vya dola. Uamuzi huo, ambao ulikuwa ghafla, ulipokewa kwa mshituko mkubwa na wadau mbalimbali, huku wengi wakihoji mwelekeo wa demokrasia nchini. Wadau hao wa kada mbalimbali, wakiwamo wanasheria, wanataaluma, wanahabari, wanaharakati, wanasiasa na watetezi wa haki za binadamu, wote wamekuwa na kauli moja ya kufanana.



SOURCE:http://www.udakuspecially.com/2013/10/afrika-kusini-yaguswa-kufungiwa-kwa.html






























 
HALI ya amani katika mji wa Mombasa imezidi kuwa tete kutokana na makundi ya vijana wenye hasira kali kuendeleza machafuko katika sehemu mbalimbali vya mji huo.


Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na BBC, jumla ya watu wanne wamepoteza maisha katika machafuko hayo, baada ya makundi ya vijana hao kupambana na askari wa kutuliza ghasia.


Habari kutoka nchini humo zinaeleza kuwa machafuko hayo yametokea siku moja baada ya kifo cha Sheikh Ibrahim Omar ‘Rogo’, aliyeuawa kwa kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana.

Katika shambulizi hilo, pia washirika watatu wa Sheikh Rogo nao wamepoteza maisha papo hapo, huku Salim Adbi akinusurika katika shambulizi hilo.

Kwa mujibu wa taarifa zaidi kutoka mjini Mombasa, vijana wenye hasira kali wameteketeza kanisa moja katika ghasia za juzi. 

Sheikh Ibrahim Rogo alikuwa mhubiri katika msikiti ambao ulikuwa unatumiwa kwa mahubiri na marehemu Sheikh Aboud Rogo, ambaye pia aliuawa kwa kupigwa risasi na watu wasiojulikana mwaka jana.

Sheikh Aboud Rogo alishutumiwa kutoa mafunzo yenye itikadi kali yaliyowashawishi vijana kujiunga na kikundi cha kigaidi cha Al Shabaab.

Kabla ya kifo chake, marehemu Aboud Rogo alidaiwa kuwa na uhusiano na kundi la kigaidi la Al Shabaab.

Tukio la kifo cha Sheikh Ibrahim Omar ‘Rogo’ limetokea ndani ya kipindi cha wiki mbili baada ya shambulizi la kigaidi la Westgate Mall, ambapo jumla ya watu 67 walipoteza maisha.


Ibrahim Rogo alionekana kama mrithi wa marehemu Aboud Rogo, alipohutubu katika msikiti huo.

Imeandikwa na Mtanzania
SULUHU ya bila kufungana kati ya Coastal Union na Azam FC katika uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga imezidi kuwaongezea idadi ya suluhu Wagosi wa kaya katika Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.


Mchezo huo uliokuwa na presha kubwa kwa mashabiki na wachezaji ulimuweka katika wakati mgumu mwamuzi Andrew Shamba kutoka Pwani, kutokana na kushutumiwa kuwapendelea Azam FC.

Kipindi cha kwanza timu zote zilicheza kwa nguvu zikihakikisha zinapata mabao ya mapema na kujihakikishia ushindi lakini hakuna hata timu moja iliyofanikiwa kuona lango la mwenzake.

Kipindi cha pili kilianza kwa Azam FC kushambulia kwa kasi huku wakimiliki mpira hali iliyowachanganya wachezaji wa Coastal Union wakaanza kupoteana na kucheza bila kufuata mfumo. Hali hiyo ilizidi kuwachanganya Wagosi wa Kaya hasa baada ya mwamuzi kuanza kutoa maamuzi ya utata, kwani katika dakika ya sabini alitoa kona kwa Azam wakati ilikuwa ni goal kick.

Mashabiki wakaanza kuhamaki na kutaka kuvuruga mchezo baada ya mwamuzi kuzidisha kutoa maamuzi ya utata kama faulo zisizoeleweka na kona za utata. Hali hiyo ilimtisha mwamuzi na kusimamisha mchezo mara kwa mara ili kuwataka wasimamizi wa mchezo huo kuwatuliza mashabiki.

Tukio lililotokea kipindi cha kwanza ambapo mwamuzi wa pembeni alipigwa na kitu kisichojulikana kutoka jukwaa la 'Rasha' lilitaka kujirudia kipindi cha pili baada ya chupa na mawe kutupwa uwanjani baada ya mwamuzi kutoa faulo nje kidogo ya 18 upande wa Coastal Union.

Dakika ya 65 mwalimu Hemed Moroco alifanya mabadiliko na kumtoa Pius Kisambale akaingia Suleiman Kassim 'Selembe'. Mabadiliko hayo yaliongeza uhai kwa Wagosi hasa kutokana na aina ya uchezaji wa Selembe kutumia mipira ya kasi.

Azam FC walianza kuelemewa kutokana na Mganda, Yayo Kato kutumia vema mwili wake mfupi na wenye nguvu kuwashambulia mabeki wa Azam, hali hiyo iliwafanya Azam kubadilika na kucheza mpira wa hovyo uliowapa nafasi Coastal Union kupiga mipira mirefu ambapo ilipofika dakika ya 75 kipindi cha pili katika jukwaa la African Sports, Wagosi walikosa bao la wazi baada ya Selembe kupiga krosi iliyopenya ngome ya Azam akiwemo mlinda mlango Mwadini Ally na kugonga mwamba.

Kutokana na piga nikupige ya lala salama kufika dakika ya 74 mwamuzi alimnyooshea mlinzi wa kulia wa Coastal Union, kinda Hamadi Juma 'Basmat', kadi nyekundu baada ya kubadilishiana maneno na mchezaji wa Azam, Kipre Tchetche.

Tukio hilo lilianzia kwa Kipre kumpiga Hamadi kiwiko cha shingo hali iliyomfanya kinda huyo kumfuata kwa jazaba huku akimuuliza kwanini amemfanyia hivyo. Mwamuzi baada ya kuona Hamadi amemuelekezea kichwa Kipre akadhani kinda huyo anapigana ndipo akatoa kadi ya moja kwa moja.

Baada ya kadi hiyo hali ya uwanja ilichafuka ambapo mashabiki walikuwa wakipiga kelele huku wachezaji wakitaka kupigana, ndipo mchezaji mwingine wa Coastal Union beki wa kushoto Othman Tamim akapewa kadi ya njano papo hapo.

Baadaye mchezo ulirudi katika hali yake lakini ngome ya Coastal Union ilikuwa imepwaya hali iliyomfanya Juma Said 'Nyoso' kuwa na kazi kubwa ya kuhakikisha ngome yao inakuwa imara.

Ilipofika dakika ya 84 mwlimu Moroco alifanya mabadiliko kwa kumtoa Uhuru Suleiman na kumuingiza Yusuf Chuma. Ambapo kinda huyo alionyesha uwezo mkubwa na kurudisha uhai wa safu ya ulinzi.

Mpaka mwamuzi wa leo anapuliza kipyenga cha mwisho matokeo yaliendelea kusomeka hivyo hivyohivyo 0-0, na kuendelea kuibakisha Coastal Union katika nafasi ya nne ikiwa na point 11 nyuma ya Azam iliyo nafasi ya tatu yenye point 11 lakini ikiwa na mabao mengi ya kufunga.

Baada ya mechi ya leo Coastal Union itashuka dimbani wiki ijayo katika uwanja wa Chamazi dhidi ya Ashanti United wanaoshika mkia katika ligi.

Hakuna maoni: