Jumatatu, 9 Septemba 2013

18 wauawa kwenye makabiliano na Boko Haram

Makundi ya vijana yanasaidia jeshi kutoa ulinzi kwa raia Nigeria

Takriban watu 18 wamefariki kwenye makabiliano makali kati ya kundi la wapiganaji wa kiisilamu la Boko Haram na kundi la kijamii la kutoa ulinzi kwa raia, katika jimbo la Borno Kaskazini Mashariki mwa Nigeria.
Wengi wa wale waliouawa waliaminika kuwa vijana wanaotoa ulinzi kwa wanavijiji waliokuwa wanatoa ulinzi kwa mji wa Benisheik dhidi ya wapiganaji wa kiisilamu.
Makabiliano hayo yametokea siku chache baada ya
jeshi kufanya mashambulizi dhidi kambi za Boko Haram na kuwaua wanamgambo 50.
Boko Haram linataka kuwepo kwa sheria za kiisilamu kote nchini Nigeria.
Kundi hilo limekuwa likifanya mashambulizi mabaya sana tangu mwaka 2009, ambayo yamesababisha vifo vya maelfu ya watu.
Lakini mashambulizi ya aina hiyo yameongezeka zaidi katika siku za hivi karibuni licha ya jeshi kupeleka wanajeshi wake katika maeneo yaliyoathirika zaidi.
Katika kujibu ongezeko la mashambulizi yanayofanywa na kundi hilo, Rais Goodluck Jonathan alitangaza sheria ya hali ya hatari katika majimbo matatu Kaskazini mwa nchi mnamo mwezi Mei likiwemo jimbo la Borno.
Fauka ya hayo, jeshi limeunga mkono ongezeko la makundi ya kutoa ulinzi katika majimbo hayo ili kukabiliana na Boko Haram.

Hakuna maoni: